Thursday, 8 March 2018

HADITHI FUPI FUPI Na. 3 - MUDA WA KIFO NI SAA MOJA NANUSU

JINA: MUDA WA KIFO NI SAA MOJA NANUSU
Mtunzi: Isihaka "Nukta" Kibao


Nilikuwa napiga hatua kidogo kidogo huku nikiwa sijali vumbi wala vijiwe jiwe vilivyokuwa vinaniumiza wakati nikivikanyaga huku viatu vyangu vikichafuka kwa vumbi la mwendo mrefu, pamoja na fujo za mtaa ule za watoto kucheza mpira wa miguu huku wakiwa wamechimbia miti ardhini kama magoli, wanawake upande wa pili wakiwa wamejikusanya wakisukana wakiwaonya wale watoto kutowapiga na mpira, wengine wakiendesha baiskeli kwa kufanya njonjo lakini akili yangu yote haikuwa katika mazingira yale.

Kilichokuwa akilini mwangu ilikuwa ni mawazo ya harusi ya msichana Belinda. Kwanini imepita kwa mtindo ule, na kwanini alinifanyia vile? Nilijiona ni kiumbe nisiye na thamani pale mjini. Mtaa ule wa fujo niliweza kuupita kwa huruma ya Mungu kutokana na fujo zake kwani nilikuwa mfano wa kivuli kiasi watu kutonijali wala kunigonga na aidha mpira au baiskeli za watoto.

Baada ya kuuvuka mtaa ule salama salmini nikamkumbuka Shukuru ambaye alikuwa ni kaka wa Belinda. Nikaingiza mkono mfukoni na kutoa simu ili nimpigie, kwani yeye ndiye angeweza kunipa maelezo stahiki ya harusi ile. Mara ghafla nikaona gari imepita kwa kasi huku ikiuelekea mtaa ule wa fujo. Nikajiuliza ni nani awezaye kuendesha kwa fujo namna ile kwenye mitaa iliyojaa watu, haikupita dakika moja nikaskia kishindo na makelele ya akina mama. Mawazo yote yakaniruka na ikanibidi kuelekea kwenye eneo la tukio kushuhudia nini kinaendelea.

Kwa kuwa sikuwa mbali nikafika pale mara moja na kuona watoto na wale akina mama wamezungukia kitu katikati, akili yangu ikanipa ni ile gari imesababisha ajali mahala pale. Sikuwa mbali na ukweli kwani ilikuwa ajali na mtoto wakiume mmoja alikuwa amegongwa. Baada ya kuona vile nikafanya haraka kuingia katikati ya kundi lile na kutoa msaada kwa kumpatia yule mtoto huduma ya kwanza na kuwaamuru wasogee mbali kidogo ili mgonjwa apate hewa safi kwani alikuwa amelala chali na damu zikimtoka upande wa sikio la kushoto.

Kuangalia kwa pembeni, aliyesababisha ile ajali alikuwa ni kijana mdogo ambaye alikuwa ameshikwa na butwaa asijue la kufanya, maana watu walimzonga huku wakimzogoa. Mara akatokea mtu mzima mmoja wa kiume ambaye alijulikana kuwa ndiye mzazi wa yule mtoto, akiwa na wasiwasi mkubwa juu ya hali ya mwanae. Ndipo nikamueleza kuwa Mimi ni Dokta na yambidi afanye haraka kumuwahisha mtoto hospitali. Yule aliyesababisha ajali ikambidi abebe jukumu la kumpeleka mtoto hospitali, nami baada ya kuona hali ile ikanibidi niingie garini ili nikatoe msaada zaidi.

Tulifika Hospitali ya Rufaa ya Bombo (Tanga) saa moja na dakika tano usiku. Nami nilivyoingia pale, muuguzi Maria baada ya kuniona tu akanisalimu

“Dr. Kera, kwema? Mbona umerudi uko hai hai…”  

Nikamwambia

“Nina mgonjwa na yambidi niingie nae chumba cha watu mahututi”

Hivyo akafuatilia kitanda mara moja cha kumbebea mtoto yule, huku mimi nikienda chumba cha madaktari kujiandaa ili kuokoa maisha ya mtoto yule. Tunaingia chumba cha watu mahututi ni saa moja na dakika ishirini na tano.

Tunaanza uchunguzi wa mgonjwa yule, kitu cha kwanza tunagundua damu nyingi zimemtoka sikioni na kwa upande wa uchogoni inaonekana kuna ubonyeo kana kwamba alijipigiza na uchogo alivyoanguka. Baada ya uchunguzi huo wa awali, namwagizia mhudumu Rukia alete mashine ya kupumulia ndipo tunagundua mgonjwa wetu yule hapumui tena kwani mashine ile haikufanya kazi, anakata pumzi na kufariki.

Tukafanya juhudi zetu za kumuokoa kwa kuushtua moyo na kumsugua kifuani ila haikufaa. Baada ya kuona vile nikarudi hatua moja nyuma na kuangalia saa, nikaona ni saa moja na nusu.
Nikafikiria itakuwa ngumu kiasi gani kwa mzazi wake kumpa habari ile, ila nikapiga moyo konde kwani madaktari ni sehemu ya kazi yetu kutoa habari za msiba kwa wahusika na nikafanya hivyo. Nikamueleza baba wa mtoto habari ile na niliushuhudia uchungu wa mtoto kwa mzazi ila ndio ilikuwa kazi ya Mungu.

Baada ya pale nikaona nijiwekeze zaidi kwenye kazi yangu na kuachana na habari ya Belinda kwani usaliti alonifanyia haukuwa wa kawaida kuchukuliwa na rafiki yangu wa karibu kipindi niko masomoni nje ya nchi.



MWISHO.


KWA HADITHI NYINGINE TAFADHALI INGIA HAPA;



No comments:

Post a Comment